TAKUKURU MKOA WA SHINYANGA YATAJA TAARIFA ZA RUSHWA, KUNA FEDHA NYINGI ZA SERIKALI ZINAPOTEA.

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga katika kipindi cha robo ya pili ya Mwaka wa fedha 2022\2023 (Oktoba hadi Disemba Mwaka 2022) ilipokea taarifa za malalamiko 52 zinazohusu rushwa 23 kutoka kwenye sekta mbalimbali ikiwemo Afya, maji, elimu pamoja na serikali za mitaa.

Taarifa hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Bwana Donasian Kessy wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema katika kipindi hicho dawati la uchunguzi limepokea taarifa za rushwa 23 na kwamba uchunguzi wake unaendelea huku taarifa zisizohusu rushwa ni 29.

Mkuu wa TAKUKURU huyo amefafanua zaidi ambapo amesema taarifa za rushwa zinazohusu serikali za mitaa 10, Elimu 5, Afya 2, Maji 2, Mahakama 2, Mazingira moja (1) pamoja na ujenzi taarifa moja (1) ambazo zote zimeanzishiwa uchunguzi.

Amesema taarifa 29 zisizohusu rushwa upande wa Ardhi taarifa sita (6), serikali za mitaa 5, Fedha 3, Elimu 3, Polisi 3, Mahakama kesi moja, Afya kesi 2, Madini kesi 2, Maliasili kesi 2, pamoja na ujenzi kesi 2 ambapo watoa taarifa hizo walishauriwa mahali sahihi pa kupeleka taarifa hizo.

 Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy amesema taasisi hiyo imefanya uchambuzi wa mfumo kuhusu uendeshaji wa masoko ya Biashara katika Manispaa ya Kahama na kubaini kuwa fedha nyingi za serikali zinapotea katika mfumo wa upangishaji vibanda na meza za biashara kwenye masoko.

“Uchambuzi wa mfumo kuhusu uendeshaji wa masoko ya biashara katika Manispaa ya Kahama tulibaini kuna fedha nyingi za serikali zinapotea katika mfumo wa upangishaji vibanda na meza za biashara kwenye masoko baadhi ya watendaji kwa kushirikiana na kamati za masoko wamekuwa wakihodhi vibanda na meza kwa kutumia majina ya wengine na kisha kuvipangisha kwa bei ya juu”.

“TAKUKURU imebaini uwepo wa wafanyabiashara wapatao 234 katika soko la CDT ambapo hawalipi kodi au ushuru kwa Manispaa hivyo kuchangia kushuka kwa mapato ya Manispaa, tumebaini uwepo wa changamoto ya kamati kukusanya ushuru kwa kutumia risiti za mikono badala ya POS lakini pia tumebaini changamoto ya mikataba iliyoingia Manispaa juu ya uzoaji wa taka kutojulikana kwa kamati za soko, TAKUKURU tumebaini pia uwepo wa changamoto za masoko kutokujua kiasi gani cha bajeti ya Manispaa kinachorudi katika kuboresha miundombinu ya masoko na huduma nyinginezo katika utendaji wa masoko”. Amesema Kessy mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga

Mkuu huyo wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy amesema hatua mbalimbali zilichukuliwa huku akieleza changamoto zilizobainika kwenye uchambuzi wa mfumo kuhusu ununuzi na ugawaji wa madawa Hospitali ya Wilaya, vituo vya Afya pamoja na Zahanati katika Manispaa ya Kahama.

“Tumebaini watumishi wa idara ya Afya hawajazi kumbukumbu za ununuzi na ugawaji wa dawa na vifaa tiba jambo linalosababisha mianya ya rushwa, tumebaini kwenye vituo vya Afya na Zahanati kuwa na uratibu wa kuazima (Kuomba dawa) hasa vituo vya jirani ambazo zinachepushwa na wala haziingii katika kumbukumbu lakini pia uwepo wa madawa yanayoagizwa muda wa matumizi (expiry date) ukiwa umefikia au umekaribia kufika, TAKUKURU tulibaini MSD kukata fedha baadhi ya vituo bila ya mzigo husika kufika kituoni na wala invoice kusainiwa vituoni (mzigo hewa), lakini pia tulibaini kutokuwepo kwa wataalamu wanaojitosheleza katika utoaji wa dawa na vifaa tiba (kwa maana ya wafamasia na wenye utaalamu wa utunzaji wa dawa)”.amesema Kessy mkuu wa TAKUKURU Shinyanga

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy amesema katika kipindi cha robo ya pili ya Mwaka wa Fedha kuanzia mwezi Oktoba hadi Disemba Mwaka 2022 Taasisi hiyo ilijikita kufuatilia fedha za miradi ya maendeleo ikiwemo sekta ya Afya na barabara ambapo jumla ya miradi ya maendeleo kumi (10) yenye thamani ya Shilingi bilioni 3.6 (3,160,000,000) na kwamba ametaja dosari mbalimbali zilizobainika.

“Tulifuatilia mradi wa barabara ya mjini inayokwenda Old Shinyanga ambayo inatekelezwa chini ya usimamizi wa TANROAD mradi huo unathamani ya Shilingi 700,010,000 TAKUKURU tulibaini kuwa kifusi cha Subgrade layer G15 na Sub base Course G25 (stabilized with cement) kimelipwa kwa urefu wa 1,080m badala ya 1,000m na kufanya mkandarasi kulipwa pesa ya ziada ya Shilingi 12,240,000 kwa kazi ambazo hazijafanyika”.

“Tulibaini pia hali ya ubora wa barabara ya mchepuko (dirvesion road) siyo nzuri na inaathiri watumiaji lakini TAKUKURU kuna hatua mbalimbali tulichukua”.ameeleza mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy

Aidha TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga imeridhishwa na ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari yaliyojengwa mwaka 2022 chini ya serikali ya awali ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mkoa wa Shinyanga ulipatiwa jumla ya Shilingi bilioni 6.6 (6,640,000,000) kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 332 ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa kitaifa wa ujenzi wa madarasa 8,000 ya shule za sekondari ambapo ujenzi wa madarasa hayo ulitakiwa kukamilika kufikia Disemba 30, 2022.

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy amesema taasisi hiyo ilifanya ufuatiliaji wa Fedha hizo kwa kutembelea kila shule iliyopatiwa Fedha ili kuhakikisha Fedha zinatumika kama ilivyokusudiwa na miradi inakamilika kwa wakati na ubora unaotakiwa.

Amesema TAKUKURU ilifuatilia utekelezaji wa ujenzi wa madarasa 158 yenye thamani ya Shilingi bilioni 3.1 (3,160,000,000) na kwamba TAKUKURU haijabaini dosari mpaka sasa ambapo ufuatiliaji bado unaendelea.

Bwana Kessy amesema TAKUKURU imeweka mikakati mbalimbali ya utendaji kazi kwa kipindi cha Januari hadi Machi Mwaka huu 2023 ikiwemo kuitangaza program ya TAKUKURU – Rafiki iliyoanzishwa na taasisi hiyo ili kuongeza ushiriki wa kila mwananchi na wadau katika kukabili tatizo la rushwa ikiwa ni sehemu ya utoaji wa huduma kwa jamii na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Bwana Donansian Kessy ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kuendelea kutoa ushirikiano kwa srikali ili kuhakikisha miradi yote inayoondelea katika Mkoa wa Shinyanga inakamilika kwa ubora.

“Kama mtaona kuna vitendo vyovyote ambavyo vinaashiria ubadhilifu wa fedha za miradi toeni taarifa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa kwa kufika ofisi zetu zilizopo Shinyanga au piga simu namba 0738150196 au 0738150197, kwa ofisi ya Kahama piga simu namba 0738150198 na ofisi ya Kishapu piga simu namba 0738150199”.amesema Kessy

TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga inawashukuru wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga hasa wale waliokaribu na maeneo ambapo miradi inatekelezwa kwa kutoa taarifa wanapoona utekelezaji wa miradi unawapa mashaka.

Mkurugenzi wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Bwana Donasian Kessy akitoa taarifa ya utekelezaji katika kipindi cha robo ya pili ya Mwaka wa Fedha 2022\2023 

(Oktoba hadi Disemba Mwaka 2022)