SIKU YA MAJI DUNIANI, WANANCHI SHINYANGA WAIPONGEZA SHUWASA, AFISA MAHUSIANO NSIANELI TUMETOA OFA KWA WATEJA WOTE

 

 Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Kuelekea kilele cha maadhimisho ya siku ya Maji Duniani baadhi ya wananchi katika Manispaa ya Shinyanga wamepongeza huduma zinazoendelea kutolewa na Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira  Shinyanga SHUWASA huku wakitaja baadhi ya changamoto zinazowakabili.

Wananchi hao wametoa pongezi hizo  leo wakati wakizungumza na Misalaba Blog kwa nyakati tofauti kuelekea maadhimisho hayo.

Wamesema kuwa wanaendelea kupata huduma ya maji lakini bado zipo changamoto zinazohitaji ufumbuzi ili kuwasaidia wananchi kuendelea kunufaika na huduma hiyo na kwamba wameiomba Mamlaka hiyo kuboresha zaidi huduma ya maji safi na salama kwa wananchi sambamba na  kutatua changamoto ya  bili za maji.

Kwa upande wake  Afisa Mahusiano na mawasiliano kutoka Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Shinyanga SHUWASA, Bi Nsianeli Gerald amewataka  watumiaji wa huduma hiyo kutoa taarifa pale  inapotokea changamoto ili ishughulikiwe haraka.

Akizungumzia siku ya maji Duniani Bi Nsianeli amesema mamlaka hiyo tayari imefuta faini za wateja waliokatiwa maji na badala yake watalazimika kulipa madeni yao kwa makubaliano.

Kesho ni kilele cha maadhimisho ya wiki ya maji Duniani ambayo ilizinduliwa rasmi Machi 16, Mwaka huu ikiongozwa na kaulimbiu inayosema “kuongeza kasi ya mabadiliko katika sekta ya maji kwa maendeleo endelevu ya uchumi”.