WADAU WA KUPINGA UKATILI WAIFIKIE JAMII, SOKO KUU SHINYANGA LIPEWE JINA DKT. JOMAARY SATURA

 

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Mwenyekiti wa mtaa wa Miti mirefu uliopo kata ya Mjini katika Manispaa ya Shinyanga Bwana Nassor Warioba ametoa wito kwa wadau mbalimbali wanaopinga vitendo vya ukatili kuifikia zaidi jamii ili kutokomeza vitendo hivyo hasa kwa wanawake na watoto.

Ametoa wito huo leo baada ya kutembelewa na Misalaba Blog ambapo amesema ili kutokomeza vitendo vya ukatili vinavyoendelea kufanyika, jamii inapaswa kuendelea kupatiwa elimu ya kutosha juu ya vitendo hivyo.

Bwana Warioba amezishauri taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuiunga mkono serikali katika mapambano ya kupinga na kutokomeza vitendo hivyo kwa kuifikia jamii zaidi kwa  kutoa elimu sahihi ya vitendo hivyo kuanzia ngazi ya familia.

Wakati huo huo Bwana Warioba ametumia fursa  hiyo  kuwaasa wananchi wa mtaa huo kutoa taarifa za wahalifu na uhalifu ili kusaidia  kuimarisha ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao.

Aidha Mwenyekiti Warioba ametumia nafasi hiyo pia kupongeza juhudi zinazofanywa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Dkt. Jomaary Satura kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa miradi ya maendeleo.